ZINGATIA HAYA UNAPOFUNGA KWARESIMA


Utangulizi


Moja kati ya mambo yanayoambatana na kipindi cha Kwaresima ni kufunga. Pamoja na hili pia kuna kusali, kutoa sadaka, kufanya toba na kushiriki matendo ya huruma. Katika kipindi hiki waamini tunaalikwa kufunga kama sehemu ya majuto na toba kutokana na dhambi zetu tulizozitenda. Katika  maana pana kufunga ni moja kati ya njia za kutafuta ukaribu zaidi na Mungu. Kufunga ni kujinyima chakula, maji, vitu au mambo ya kidunia kwa utukufu wa Mungu.

Sheria juu ya kufunga


Ni Amri ya kanisa kufunga siku ya Jumatano ya majivu na kutokula nyama siku ya Ijumaa kuu. Vivyohivyo katika sheria za kanisa, sheria namba 1250 mpaka 1252 zinaeleza kuwa Ijumaa zote pamoja na kipindi cha kwaresima ni siku za toba. Vijana wa kuanzia umri wa miaka kumi na minne mpaka wazee wa umri wa miaka sitini wana wajibu katika kanisa wa kufunga na kujinyima katika siku hizo za toba. Ungalizi wa kanisa na wazazi unahitajika kuwaeleza watoto maana haswa ya kufunga. Hali kadhalika wazee, wajawazito, wagonjwa pamoja na watu wenye mahitaji maalum hawabanwi na sheria hizi.
Mambo yafuatayo ukiyazingatia utapata thawabu katika kufunga kwako

      Funga ukiwa umweka nia, usifunge kwa kuwa ni sheria.


Ni kosa kubwa kuamua kufunga kwa kuwa tu hiki ni kipindi cha kwaresima kila mtu anafunga nawe ukaamua kufunga. Kufunga kunahitaji kwanza kuweka nia, kutambua kwa nini unafunga.
  1. Je unafunga kuomba msamaha?
  2. Au uanfunga kwa ajili ya kupeleka maombi maalum?
  3. Au unafunga ili upate ukaribu na kusikia sauti ya Mungu?
  4. Au unafunga ili upate wasaa wa kutafakari na Mungu ukuu wake katika katika maisha yako?
  5. Nakadhalika

Hakikisha una nia madhubuti ambayo unataka kuitimiza usifunge kwa kufuata mkumbo, maana kufunga kwako hakutakuwa na maana.
Ukishaweka nia yako hii ya kufunga, mshirikishe Mungu na uombe msaada wa Mama Bikira Maria kukusaidia katika kufunga na kuitimiza nia yako.

      Kufunga kunaenda na sala.


Unapoamua kufunga unatengeneza ukaribu na Mungu, naye yupo tayari kukusikiliza muda wote. Hivyo unapofunga ni wakati wa kusali sana, ni wakati wa kuzungumza na Mungu. Unapoianza siku, mueleze Mungu katika maombi ni kwa nini unafunga na umuombe akusaidie katika kufunga kwako, katikati ya siku mkumbushe Mungu na hata jioni unapoihitimisha funga yako mshukuru Mungu kwa kukusaidia kuhitimisha salama.
Na usalipo usisali sala ya kibinafsi, usipeleke maombi yako peke yako kwa Mungu. Omba kwa ajili ya ulimwengu mzima, Sali pia kwa ajili ya wale wasiomjua Kristo bado, vivyo hivyo sali pia kwa ajili ya wale wasio na mwombezi.

      Kufunga Kunaenda na Ibada.


Ili funga yako ya kwaresima ikamilike lazima iambatane na ibada mbalimbali zinazotolewa na kanisa. Ibada hizi hujumuisha Njia ya Msalaba, Kuabudu Ekaristi, Rozari takatifu, Ibada ya Misa takatifu nakadhalika. Ibada hizi hukusaidia kukusogeza karibu zaidi na Mungu, nazo hukupa nafasi ya kumtafakari Mungu katika mafumbo yake makuu na ya kustaajabisha.

       Kufunga huendana na Tafakari.


Kama nilivyoeleza awali kuwa unapofunga lazima ujiwekee lengo. Hivyo wakati unaendelea na mfungo mara kwa mara lazima ufanye tafakari juu ya lengo lako ulilojiwekea. Je, kuna maendeleo yoyote, kama hakuna maendeleo tatizo ni nini? Pia tafakari juu ya kufunga kwako kama uanenda sambamba na jinsi ambavyo kanisa linawaelekeza waamini kufunga.

      Kufunga huenda na toba na kusamehe.


Yamkini lengo lako kuu la kufunga sio kutubu, labda kuna maombi maalumu unataka kuyapeleka kwa Mungu lakini kabla ya yote unapaswa kwanza kujichunguza na kufanya toba pamoja na kuwasamehe wale wote ambao wamekukosea. Ukifanya hivyo funga yako pamoja na maombi vyote vitapokelewa kwa Mungu.

       Usifunge kama wanafiki.


Yesu mwenyewe katika Mathayo 6:13-18 anawaonya wanafunzi wake kwamba wafungapo wasiwe kama wanafiki ambao hukaa na nyuso za kukunjamana kuonesha kuwa wamefunga. Kumbuka kuwa unatafuta ukaribu na Mungu, yeye aliyesirini anayeona moyo wako. Ukijionesha kwa watu ili upate sifa haifai kitu. Kumbuka kuwa lengo lako la kufunga halikua kujionesha kwa watu.

           Kufunga kuna ambatana na sadaka na matendo ya huruma.


Unapofunga unajinyima na kujikatalia kwa Utukufu wa Mungu, kiasi ya fedha unachoacha kutumia si mali yako. Hivyo ili funga yako ikamilike kiasi hicho inabidi ukipeleke madhabahuni kama sadaka au uende ukafanye matendo ya huruma. Endapo utaitumia fedha uliyoipata kwa kutonunua mahitaji yako wakati umefunga ni sawa na kuwa uliahirisha kujistarehesha kwa kipindi fulani wala si kwamba ulifunga.

NIKUTAKIE MFUNGO MWEMA



Je kuna jambo ambalo unadhani ni muhimu kuongezwa katika orodha hii AU kuna jambo ambalo ungependa niliandikie; Usisite niandikie kupitia benedict.temba@gmail.com au nitumie ujumbe kwenye 0712135209 nami nitawashirikisha wengine


Popular posts from this blog

IFAHAMU SAKRAMENTI YA KITUBIO/UPATANISHO

IFAHAMU SALA YA BWANA (BABA YETU)

NYIMBO ZA BIKIRA MARIA