Je wewe ni Simeoni wa Kirene? (Tafakari)

Tunasoma katika Injili ya Mtakatifu Marko 15:21, habari za Simeoni wa Kirene aliyemsaidia Yesu msalaba. Ni mstari mmoja tu, lakini wenye maana kubwa sana katika Imani. Kanisa kwa kutambua mchango wa mstari huu mmoja, umetenga kituo cha tano katika Ibada ya njia ya msalaba, kutafakari fumbo hili kubwa.
Nataka nikukaribishe tuutafakari mstari na fumbo hili la Simeoni wa Kirene anayemsaidia Yesu Msalaba.

  • Mazingira ya tukio

Simeoni alikua anatoka shambani kuelekea nyumbani kwake. Yamkini hakua anafahamu ni jambo gani linaloendelea wakati ule, au kama alikua anafahamu basi halikua jambo la msingi sana kwake. Maana kama angekua ni mwamini au mwanafunzi wa Yesu Kristo asingekua anatokea shambani wakati ule, lazima angekua katika hali ya huzuni na majonzi. Simeoni yamkini alisogea katika msongamano ule wa safari ya kuelekea Kalivari baada ya kuona mkusanyiko mkubwa wa watu, ni hulka ya binadamu kupenda taarifa. Labda alijongea ili kujua ni nini kinaendelea.

Lakini ghafla, anashurutishwa kumsaidia Yesu kuubeba msalaba. Simeoni anapewa kazi ya kushiriki adhabu, mateso na machungu na mtu asiyemfahamu. Simeoni anakubali, labda kwa kufuata amri ya askari lakini pia labda kwa huruma anayoiona juu ya Yesu ambaye alikua yu dhoofu hali.

Simeoni anashiriki kazi ya ukombozi kwa kuubeba msalaba pamoja na Kristo, jambo lile limeweka jina lake katika historia ya kanisa duniani, na limeandikwa hivyo pia katika mbingu. Je, Simeoni wa Kirene ni zawadi gani atayostahili kubwa zaidi ya kushiriki katika meza ya Bwana milele?

  • Funzo katika fumbo hili

Simeoni, alifanya jambo moja la upendo na ukarimu. Hakujua zawadi itakayotokana na msaada ule. Simeoni alikua anatoka shambani, lazima alikua amechoka. Lakini aliuona uchovu wake kuwa si kitu mbele ya Kristo aliyekua amevia damu mwili mzima, Yesu ambaye mwili wake umechakaa kutokana na mateso. Tendo lake moja la ukarimu, tena bila kufahamu malipo yake limempa Simeoni nafasi kubwa sana katika historia, katika kanisa na zaidi ya yote katika Mbingu.

  • Wewe pia ni Simeoni wa Kirene


Kila wakati unapokutana na mtu mwenye kuhitaji msaada wako, wewe unakua Simeoni wa Kirene. Yawezekana umetoka shambani namaanisha ukawa umechoka labda huna fedha, huna nguvu, umebakiwa na akiba ndogo sana nakadhalika. Yamkini mtu anayehitaji msaada wako ni hohehahe wa kutupwa na watambua hakuna namna ambavyo anaweza kukulipa.

Kumbuka Simeoni wa Kirene alibeba msalaba na Yesu akiwa ametoka Shambani na amechoka haswa. Alibeba msalaba wa mtu anayeenda kufa, hivyo alijua hatopata chochote, aliubeba msalaba kwa ukarimu na upendo. Vivyo hivyo nasi katika kuombwa msaada, tusijali kuwa tumechoka wala tusitafute faida gani tutaipata kutokana na kusaidia. Tuwasaidie watuombao msaada, pamoja na uchovu wetu, tuwasaidie bila kuangalia wataturudishia nini.

Tuufuate mfano wa Simeoni wa Kirene.

Popular posts from this blog

IFAHAMU SAKRAMENTI YA KITUBIO/UPATANISHO

IFAHAMU SALA YA BWANA (BABA YETU)

NYIMBO ZA BIKIRA MARIA