Kwaresima: Jifunze, Tafakari juu ya fumbo la Shamba la Mizabibu (Isaya 5:1-7)

Katika Isaya 5:1-7, Nabii Isaya, anaeleza fumbo fupi kupitia kisa cha shamba la mizabibu.


  • Kisa cha Shamba la Mizabibu?

Anaeleza; Mkulima alikua na shamba la mzabibu, mahali pa kilimani penye kuzaa sana, kwa kulijali akalipalilia, akalisafisha, akaweka samadi iliyo nzuri, akalitengenezea na kisima cha maji ndani yake. Akitegemea kuwa litazaa zabibu zilizo njema na safi lakini likazaa zabibu mwitu, zabibu chungu. Kisha anauliza akisema; Je, ni jambo gani nililopaswa kulitenda katika shamba langu la mizabibu na sikulifanya? Mbona nalipotegemea litazaa zabibu safi limezaa zabibu mwitu?

  • Fumbo hili lina maana gani?

Mkulima ni Mungu, na shamba la mizabibu ni sisi binadamu kila mmoja kwa nafasi yake. Kazi aliyoifanya mkulima ya kuliandaa shamba la mizabibu ni zawadi, vipawa, na talanta ambazo Mungu ametujalia. Zabibu ni matunda yatokanayo na zawadi, talanta na vipawa ambavyo Mungu ametujalia.

  • Fumbo hili lina uhalisia gani?

Katika maisha yetu Mungu ametubariki katika namna mbalimbali, kila mmoja kwa namna yake binafsi. Tumejaliwa uhai, elimu, vipaji, hekima, talanta, umaridadi nakadhalika. Kutoka katika mambo yote hayo Mungu aliyotujalia anategemea tutoe matunda safi na yenye kupendeza. Anataka tuifundishe jamii njia yake, tuwasaidie watu kwa upendo, tushiriki katika uenezaji wa injili, tuwafariji wanaaonewa na kudharauliwa. Mungu anategemea tutumie zawadi zake katika kumtukuza yeye. Lakini sisi tumekengeuka, tunatumia zawadi za Mungu kumtukuza shetani.

  • Tafakari binafsi

Jaribu kufikiri kila zawadi ambayo Mungu amekupatia ni kwa namna gani unayoitumia? Jiulize pia kwa namna ambavyo unayaendesha maisha yako je sifa zinaenda kwa Mungu ama hasha!

  • Fumbo hili lina maana gani katika kipindi hiki

Kipindi cha kwaresima ni wakati wa kujitafakari na kuangalia wongofu.  Tunaalikwa kujitafakari kama ni kweli tunatoa matunda kulingana na nguvu ambayo Mungu amewekeza juu yetu. Endapo tutang’amua ya kuwa hatutoi matunda yenye kumpendeza Mungu hima tukimbilie katika kiti cha kitubio na kuomba toba.

  • Tusipobadilika nini kitatokea?


Majibu yanaonekana katika Isaya 5:5-6, ataliharibu shamba la mizabibu na ataacha likanyagwe na hatalitunza tena. Hii ni adhabu kubwa mno, maana Mungu ataondosha baraka zake juu yako naye atakuacha ukiwa bila rutuba, matokeo yake ni mahangaiko na mateso makuu. Tusifike huku, tumuombe Roho Mtakatifu atuongoze vyema na atuasaidie kuishika ile iliyo kweli.

Kwaresima njema.

Popular posts from this blog

IFAHAMU SAKRAMENTI YA KITUBIO/UPATANISHO

IFAHAMU SALA YA BWANA (BABA YETU)

NYIMBO ZA BIKIRA MARIA